Drawer trigger

Uislamu Chaguo Langu 15 + Sauti

Sikiliza Hamjambo wapenzi wasikilizaji na karibuni katika kipindi hiki ambacho huangazia maisha ya watu ambao baada ya kufanya utafiti wa kina, wameamua kusilimu na hivyo kufuata njia iliyojaa nuru ya Uislamu, na leo tutamuangazia Mmarekani Steven Krauss. Karibuni kujiunga nami hadi mwisho. @@@ Katika dunia ya leo, dini tukufu ya Kiislamu inazidi kuwafungulia wanaadamu upeo mpya. Uislamu umebeba ujumbe wenye kuleta mbadiliko katika kila upeo wa maisha ya mwanaadamu. Kwa kufuata Uislamu mwanaadamu anaweza kuokoka kutokana na tufani ya maisha ya leo. Steven Krauss ni Mmarekani aliyesilimu kutoka mji wa New York ambaye anasema maisha yake yalichukua muelekeo bora punde baada ya kuikumbatia dini ya Kiislamu. Anasema hivi kuhusu mabadiliko katika maisha yake: "Kila siku Uislamu unaniletea mabadiliko mapya katika maisha yangu na namshukuru Mwenyezi Mungu kwa hilo. Ni Mwislamu tu ndiye anayeweza kufahamu kilele cha rehema za Mwenyezi Mungu. Hii ni kwa sababu kila siku Mwislamu anasujudu na kujisalimisha kwa Mola muumba." Baada ya kusilimu, Steven Krauss alichagua jina la Abdullatiff Abdullah. Kwa mtazamo wake, Uislamu, kinyume na Uyahudi na Ukristo, si itikadi tu bali ni njia iliyojaa nuru ambayo humfikisha mwanaadamu katika ukweli na nguvu halisi, yaani Allah SWT. Abdullatif Abdullah anasema hivi kuhusu namna alivyouchagua Uislamu kama njia yake ya maisha: 'Nilianza kuujua Uislamu nilipokuwa mwanafunzi wa chuo kikuu. Nilikuwa Mkristo wa Kanisa la Protestanti na kwa muda mrefu nilikuwa sifuati kivitendo dini. Sikuvutiwa sana na Ukristo kutokana na kuwa dini hii haikidhi hitajio la kumjua Mwenyezi Mungu kwa dhati wala haina chochote chenye maana kuhusu uhusiano wa Mwanaadamu na Mwenyezi Mungu. Uhusiano tata na usio na muelekeo baina yangu na Mola Muumba ndilo jambo lililonipelekea kuanza kutafuta njia ambayo ingeniwezesha kuwa na uhusiano bora na Mwenyezi Mungu. Kwa nini tusimuombe Mwenyezi Mungu kwa njia ya moja kwa moja? Ni vipi Mwenyezi Mungu anajitokeza kwa umbile la mwanaadamu? Kutokana na maswali hayo nilikuwa na mtazamo wa wazi kuhusu dini na hivyo nikaanza kutafuta dini ambayo ingeniongoza kwa njia ya kweli badala ya kufuata dini isiyo na msingi wa akili na mantiki. Kujuana na Mwislamu na kushuhudia namna alivyoishi ni jambo ambalo lilijibu maswali yangu mengi na hivyo kunifungulia njia ya kuelekea katika ukweli na uhakika maishani." Utulivu wa kiakili ni moja kati ya mahitajio muhimu ya mwanaadamu wa leo duniani. Hii ni kwa sababu aghalabu ya watu katika dunia ya leo wanakumbwa na matatizo ya ukosefu wa utilivu wa kiakili na kisaikolojia. Iwapo tutachunguza chanzo cha maradhi mengi ya kisaikolojia katika jamii, tutagundua kuwa sababu muhimu ya maradhi hayo ni udhaifu katika uhusiano wa wanaadmu na Mwenyezi Mungu. Kwa mtazamo wa Mwislamu, Mwenyezi Mungu si itikadi tu bali yeye ni nguvu ya juu zaidi na wakati huo huo ana uhusiano wa karibu sana na mwanaadamu, uhusiano ambao ni wa karibu zaidi kuliko tunavyodhani. Kuhusu hili, Mwenyezi Mungu katika sehemu ya aya ya 16 ya Surat Qaaf katika Qur'ani Tukufu anasema: "Na Sisi tuko karibu naye kuliko mshipa wa shingoni mwake." Vile vile katika sehemu ya aya ya nne ya Surat al Hadiid, Mwenyezi Mungu anasema: Naye yu pamoja nanyi popote mlipo. Na Mwenyezi Mungu ni Mwenye kuyaona mnayo yatenda. Kwa hivyo kila ambaye ana uhusiano na Mwenyezi Mungu ananufaika na fadhila na rehma zake. Katika hali kama hii si tu kuwa mwanaadamu hujawa na matumaini bali pia uhusiano huu humuelekeza katika saada, amani na utulivu kama ambavyo Allah SWT anasema katika Surat Al Fat'h Aya ya Nne:  "Yeye ndiye aliye teremsha utulivu katika nyoyo za Waumini ili wazidi Imani juu ya Imani yao." Katika dunia ya leo, wanaadamu wanakabiliwa na mitihani ya vivutio vya kidunia visivyo kuwa na maana na vyenye kuangamiza. Kwa msingi huu, furaha na mafanikio yanahesabiwa kwa mizani ya utajiri na matumizi ya bidhaa za kisasa na kila ambaye ataonekana ana mapungufu katika masuala ya kifedha na kimaada huhesabiwa kuwa mwanaadamu  asiye na matumaini wala muelekeo maishani. Abdulatiff Abdullah anasema ni jambo la kusikitisha kuona katika jamii ya leo mwanaadmau akiwa amejawa utupu na batili, ambapo hafikirii chochote isipokuwa maslahi yake binafsi. Anasema: "Mimi ni mtaalamu wa sayansi za kijamii na katika taaluma yangu hii daima huwa ninachunguza maradhii ya kijamii katika jamii ya Marekani. Kufuatia uchunguzi wa kina nimefikia natija hii kuwa maradhi mengi ya kijamii yanatokana na tabia mbaya na kutokuwa na muelekeo wa kimaanawi. Kutokana na kuwa Uislamu ndiyo nidhamu bora na salama zaidi ya maisha katika jamii ya mwanaadamu, dini hii ndiyo njia pekee na ya kweli katika kutatua matatizo na migogoro ya kijamii. Nimefikia natija kuwa si tu kuwa Uislamu ni njia kamili ya maisha ya kila siku bali pia nimeweza kufahamu kuwa kuna tofauti za kimsingi kati ya Uislamu na dini nyinginezo. Uislamu ni hitajio la wanaadamu wote waliopotea. Uislamu ndiyo njia ya kufika katika lengo, maana halisi ya maisha na saada. Uislamu unamfikisha mwanaadmu moja kwa moja hadi katika chimbuko la uhakika na nguvu ya kweli yaani Allah SWT. Mmarekani huyu aliyesilimu anaendelea kusema: "Kwa hakika moja ya sababu zilizonipelekea nivutiwe sana na Uislamu ni kuwa, sambamba na kuijua dini hii nilishuhudia ilivyokuwa ikitekelezwa katika maisha ya kila siku kupitia rafiki yangu Mwislamu. Uislamu ni njia kamili ya maisha na wakati Uislamu unapoingia kikamilifu katika maisha basi haiwezekani tena kuitenganisha dini hii na maisha ya kila siku. Jambo hili ni kinyume kabisa na Ukristo ambao ni dini inayokinzana na fitra ya maisha ya mwanaadamu. Uislamu unawataka wafuasi wake kutazama kila kitu katika maisha kwa mtazamo wa Ibada." @@@ Wanasaikolojia wanatoa mapendekezo ambayo yanaweza kumletea mwanaadamu utulivu wa kiakili. Wanasema mbinu muhimu zaidi katika kutibu maradhi ya kisaikolojia ni 'dini'. Uchunguzi umebaini kuwa idadi kubwa ya wagonjwa wa kiakili wanaopata nafuu na kupona ni wale ambao wanamwamini Mwenyezi Mungu. William James, mwanafalsafa na mwanasaikolojia wa Marekani anasema: "Imani ya kidini ina nguvu ya ndani ambayo ni lazima imsaidie mwanaadamu katika maisha. Ukosefu wa imani ya kidini katika maisha ni jambo hatari ambalo humfanya mwanaadamu ashindwe kustahamili masaibu maishani.' Abdullatif Abdullah anasema baada ya kusilimu sasa amepata utulivu maishani. Anaendelea kuongeza kuwa: 'Uislamu umenionyesha ni kwa nini wanaadamu wasio na imani ya kidini wanapapta matatizo. Maisha bila kumwamini Mwenyezi Mungu ni jinamizi. Mimi nalifahamu hili vizuri kwani wakati mmoja nilikuwa katika hali hiyo lakini sasa nimepata uhuru wa kishaksia. Hivi sasa maisha yangu yamepata maana na nidhamu maalumu. Nimefahamu kwa nini nilisilimu. Nimefahamu ni vipi niishi na ninaelekea wapi. Kile ambacho ninaomba ni kuwa wote waliopotea siku moja waweze kuongoka na kupata furaha niliyonayo leo katika Uislamu.' http://kiswahili.irib.ir